Vodacom kuuza hisa; Zijue faida za kununua hisa za makampuni.

Kampuni ya Vodacom imeingia katika vichwa vya habari hivi karibuni hapa nchini baada ya kutangaza kujiandikisha katika soko la hisa la Dar es salaam la DSE.
kampuni hii ya mtandao wa simu ambayo ni moja ya mitandao yenye watumiaji wengi zaidi Tanzania unafanya hivyo ili kutekeleza sheria ya Elektroniki na Mawasiliano ya Posta (EPOCA) na sheria ya fedha ya mwaka 2016 inayoyataka makampuni ya simu kumilikisha asilimia 25 ya hisa zake kwa wananchi.
Ingawa Voda wamekuwa ni wa kwanza kuitikia mwito huu wa serikali lakini ni wazi kwamba makampuni mengine yatafuata hatua hii na kumilikisha kiasi cha mtaji wake kwa wananchi. Katika makala hii nitaandika faida chache ambazo wewe msomaji utazipata iwapo utaamua kununua hisa katika makampuni haya ya simu.
Gawio.
Makampuni mengi ambayo yameuza hisa zao huigawanya faida inayopatikana katika mwaka kwa wanahisa wote kwa kuangalia uwiano wa hisa mtu anazomiliki, hivyo unapokuwa na hisa nyingi katika kampuni ambayo inapata faida kubwa basi gawio lako linakuwa kubwa zaidi.
Thamani ya hisa zako kuongezeka.
Hisa zinaongezeka thamani kadiri ambavyo kampuni inakuwa kibiashara, hisa ambazo ulinunua kwa shilingi laki moja utakapoamua kuziuza zinaweza zikawa na thamani kubwa kushinda uliyonunulia kama kampuni imepata faida kibiashara (lakini pia inawezekana kabisa hisa ulizonunua zikaporomoka thamani iwapo kampuni haitafanya vizuri katika biashara yake).
Mwakilishi wa Vodacom akiwa na mwakilishi wa soko la hisa la Dar es salam.
Unaweza kupata bonasi ya hisa.
Ni kawaida kwa kampuni ambazo zimeuza umiliki wake kwa watu kupitia hisa kutoa bonasi ya hisa kwa wana hisa wake pindi linapokuwa limepata faida kubwa, japokuwa sio lazima lakini pindi kitu kama hiki kinapotokea basi wenye hisa hufaidika kwa kuwa wanapata hisa zaidi na hivyo kujiongezea kipato katika gawio.
Hisa huweza kutumika kama dhamana kujipatia mikopo.
Hati ya umiliki wa hisa kama ilivyo hati ya nyumba ama hati ya gari humuwezesha mmiliki wa hisa kujipatia mikopo katika taasisi ambazo zinatoa huduma hizo, hii humsaidia mwana hisa pindi anapokuwa anahitaji fedha ama mkopo.
Wamiliki wa hisa huwa na usemi juu ya mambo fulani ya husuyo kampuni.
Kampuni hufanya mkutano mkuu walau mmoja kwa mwaka ambapo wanaomiliki hisa hupitisha baadhi ya mambo muhimu ya kampuni, hii inawafanya wamiliki wa hisa katika makampuni kuweza kuwa na maamuzi ya nini kifanyike katika kampuni.
Voda pamoja na makampuni ya mengine yataanza kuuza hisa, chaguo ni lako wewe msomaji uwekeze katika kampuni ipi hasa. Hii ni nafasi kwa wale ambao walikuwa wanatamani kuwa sehemu ya wamiliki wa makampuni ya mitandao hii, hivyo kama wewe ni mmoja wa hawa basi huu ndio wakati wako kuwekeza.
Je unazifahamu faida nyingine za kumiliki hisa katika kampuni? Tushirikishe katika maoni ili wengine pia wazifahamu.

Previous
Next Post »

Ads Inside Post